Mzee Mufti anaamini anaweza kuwapenda wake zake wote kwa usawa. Lakini ndani ya kasri lake, mapenzi si hesabu rahisi. Bi. Fadhila ndiye mke wa kwanza, nyota ya nyumba na mwanamke aliyesimama naye tangu mwanzo. lla baada ya miaka mingi bila mtoto, penzi lao linaanza kupimwa na minong’ono ya majirani, shinikizo la familia na kiu ya Mzee Mufti kuitwa baba. Anapomleta Bi. Khadija, muimba taarabu mchanga mwenye uzuri, elimu na ulimi mkali, kasri hilo linaanza kuwaka kwa wivu, vijembe na mashindano ya hadhi. Kisha wanaingia wake wengine, kila mmoja na nafasi yake, ndoto zake na hofu yake ya kupoteza upendo wa mume mmoja.
“Kasri la Wake Wanne” ni tamthilia ya mapenzi, mamlaka na majeraha ya ukewenza. Kwa kutumia kanga, taarabu, methali na lugha yenye ladha ya pwani, Anna Samwel Manyanza anatufikisha ndani ya nyumba inayong’aa kwa nje, lakini ndani yake wanawake wanapambana na upweke, ushindani, uzazi, tamaa na gharama ya kupendwa kwa zamu.
KUHUSU MWANDISHI
Anna Samwel Manyanza ni mwandishi mahiri anayeandika kwa mtazamo mpana wa kidunia. “Penzi la Damu”, kazi yake ya kwanza, ilishinda Tuzo ya Kiswahili ya Safal ya Fasihi ya Afrika mwaka 2015. Pia, ana riwaya nyingine inayoitwa “Faradhi ya Moyo”. Zaidi,anaandika hekaya za watoto. Kazi yake ya kwanza katika uga huo,”Kakofia Keusi”, imefasiriwa katika lugha nyingine tatu: Küingereza (Little Black Cappy), Kijerumani (Schwarzkäppchen) na Kifaransa (Le Petit Chaperon Noir).





Reviews
There are no reviews yet.